
Mlonge (Moringa oleifera) ni mmea wenye thamani kubwa kiafya na unatumiwa kutibu na kusaidia katika kudhibiti magonjwa mbalimbali kutokana na wingi wa virutubisho na viambata vyenye uwezo wa kitiba. Makala hii imeorodhesha baadhi ya magonjwa yanayodhibitiwa au yanayotibiwa na mlonge;
Ugonjwa wa kisukari
Majani ya mlonge yana uwezo wa kupunguza viwango vya sukari kwenye damu, hivyo kusaidia wagonjwa wa kisukari kudhibiti ugonjwa huu, Tafiti zinaonyesha pia kuwa mlonge huongeza uzalishaji wa kichohceo insulini na kuboresha utendaji kazi wa kongosho, kwa kufanya hivi huweza kudhibiti kisukari.
Shinikizo la juu la damu
Mlonge una kiasi kikubwa cha potasiamu, ambacho husaidia kupunguza shinikizo la damu, potasiumu hufanya kazi ya kupanua mishipa ya damu hivyo kupelekea kushuka kwa shinikizo. Viuajisumu vilivyoshamiri katika mlonge husaidia kuimarisha afya ya moyo na mishipa ya damu.
Magonjwa ya Ini
Mlonge una viambata vinavyosaidia kulinda ini dhidi ya sumu na kuimarisha uwezo wake wa kutoa sumu mwilini. Husaidia pia kurekebisha uharibifu wa ini unaosababishwa na matumizi mabaya ya pombe au dawa.
Upungufu wa damu
Mlonge una madini ya chuma na vitamini C ambayo husaidia kuongeza uzalishaji wa chembe nyekundu za damu na hivyo husaidia wagonjwa kurejesha kiwango cha damu katika hali ya kawaida.
Magonjwa ya mfumo wa kinga
Majani ya mlonge yana vitamini C na E nyingi ambazo husaidia kuimarisha kinga ya mwili dhidi ya maambukizi. Pia yana viambata vyenye uwezo wa kupambana na bakteria na virusi.
Magonjwa ya udhaifu wa mifupa na maungio ya mwili
Mlonge una kalsiamu na fosforasi nyingi ambazo ni muhimu kwa uimara wa mifupa. Pia una sifa za kupunguza maumivu na uvimbe katika viungo.
Magonjwa ya tumbo na matatizo ya mmeng’enyo wa chakula
Mlonge husaidia kupunguza vidonda vya tumbo na gesi, na kuvimbiwa kwa kuongeza usagaji mzuri wa chakula.
Magonjwa ya ngozi
Mafuta ya mbegu za mlonge yanaweza kutumika kutibu chunusi, upele, na mikunjo ya ngozi kwa sababu yana sifa za kuwa na viuajibakteria na vizuia michomo kinga.
Saratani
Baadhi ya tafiti zinaonyesha kuwa mlonge una viambata vinavyoweza kusaidia kupunguza kasi ya ukuaji wa seli za saratani na pia husaidia mwili kuondoa sumu ambazo zinaweza kusababisha saratani.
Magonjwa ya macho
Mlonge una vitamini A kwa wingi inayosaidia kulinda macho dhidi ya matatizo kama upofu wa usiku na matatizo mengine ya kuona
Jinsi ya kutumia mlonge kwa tiba
Majani – Hutumiwa kama chai, juisi, au unga kwenye chakula.
Mbegu – Huliwa moja kwa moja au kusagwa kuwa unga kwa detox.
Mafuta ya Mlonge – Hutumika kwa ngozi na nywele.
Gome na Mizizi – Hutumiwa kwa tiba za kienyeji, lakini zinahitaji tahadhari.
Kumbuka: Kuelewa kuhusu dozi halisi na matumizi ya kitiba wasiliana na daktari wako wa tiba asili kwa ushauri.
Tahadhari
Wanawake wajawazito wanapaswa kuepuka kutumia mlonge kupita kiasi, hasa mizizi yake, kwani inaweza kusababisha changamoto kwa ujauzito.
Rejea za mada hii
Pareek A, et al. Moringa oleifera: An Updated Comprehensive Review of Its Pharmacological Activities, Ethnomedicinal, Phytopharmaceutical Formulation, Clinical, Phytochemical, and Toxicological Aspects. Int J Mol Sci. 2023 Jan 20;24(3):2098. doi: 10.3390/ijms24032098. PMID: 36768420; PMCID: PMC9916933.
Fuglie L.J. Producing Food without Pesticides: Local Solutions to Crop Pest Control in West Africa. 1st ed. Church World Service; Dakar, Senegal: 1998. pp. 1–158.
Gandji K.,et al. Status and utilisation of Moringa oleifera Lam: A review. Afr. Crop Sci. J. 2018;26:137–156. doi: 10.4314/acsj.v26i1.10.
Chaudhary K., Chourasia S. Nutraceutical properties of Moringa oleifera: A review. EJPMR. 2017;4:646–655.
Gopinath L.R., Jeevitha S., Gokiladevi T., Archaya S. Isolation and Identification of therapeutic compounds from Moringa oleifera and its antimicrobial activity. IOSR-JPBS. 2017;12:1–10.
Kasolo J.N.,et al. Phytochemicals and uses of Moringa oleifera leaves in Ugandan rural communities. J. Med. Plant Res. 2010;20104:753–757.